Falsafa Ya Mwalimu Nyerere Kuhusu Elimu

Falsafa Ya Mwalimu Nyerere Kuhusu Elimu, Miaka 24 imepita tangu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alipotuacha. Lakini je, kweli ametuacha? Kifikra, kiroho, yupo nasi. Mawazo yake, falsafa zake, viko bado hai katika mioyo na akili za Watanzania wenye mapenzi mema kwa nchi yao. Alituachia taifa salama na pia fikra zinazotuongoza, mojawapo ikiwa ni elimu.

Elimu kwa Nyerere: Si Anasa, Bali Chombo cha Mabadiliko

Mwalimu aliamini kuwa elimu ni nguzo muhimu ya maendeleo. Lakini sio elimu yoyote, bali elimu ya kujitegemea. Hii si elimu ya vyeti tu, bali ni elimu inayomfanya mwanafunzi awe na uwezo wa kusaidia kujenga taifa lake. Nyerere hakutaka elimu iwe ya kutengeneza wafanyikazi wa makampuni, bali watumishi wa jamii.

“Elimu lazima itumikie jamii,” aliwahi kusema. Kwa Nyerere, si sawa kwa serikali na wazazi kutumia rasilimali nyingi kuwasomesha vijana, halafu vijana hao wasirudi kuitumikia jamii. Fikra hii ilikuwa wazi: msomi yeyote aliyepata elimu kupitia rasilimali za taifa alikuwa na deni kubwa kwa jamii.

Elimu ya Kujitegemea: Nguvu ya Kujenga Jamii

Elimu ya kujitegemea haikuwa tu ndoto, bali ni mpango ambao Mwalimu alitaka kuuona ukitekelezwa. Aliamini kuwa taifa la watu waliosoma linapaswa kuwa na uwezo wa kuleta mabadiliko ya kweli. Vijana waliopata elimu, kupitia sera za kijamaa, walitakiwa warudi vijijini kujenga jamii mpya za kijamaa. Kwa Nyerere, elimu haikuwa njia ya kutafuta ajira bali ilikuwa ni njia ya kuijenga jamii.

Lakini miaka 21 baada ya kifo chake, tunajiuliza: je, tumeendelea na falsafa hii? Licha ya serikali na wazazi kujitoa kwa hali na mali katika kusomesha vijana wengi, wengi wao baada ya kuhitimu huishia kuwa mizigo katika familia badala ya kuwa suluhisho la changamoto za kijamii.

Wasomi na Jamii: Uhusiano Uliovunjika

Mwalimu alitaka wasomi wawe sehemu ya jamii, wachangamane na kushirikiana na watu waliowakuzia. Lakini leo hii, wasomi wengi wamejitenga. Wamejifungia kwenye minara ya pembe, wakiacha jamii iliyowasomesha ikihangaika. Hawataki kuwa sehemu ya mabadiliko, hawataki kushiriki katika kutatua matatizo ya jamii.

Elimu, kwa Nyerere, ilikuwa ni zaidi ya ajira. Ilikuwa ni utumishi kwa watu, kujitoa kwa hali na mali kwa ajili ya kuboresha maisha ya wengine. Lakini leo, tunashuhudia kinyume chake.

Kumuenzi Nyerere: Kurudisha Misingi ya Elimu

Katika kumbukizi ya miaka 24 ya kifo cha Mwalimu, tunapaswa kujiuliza: je, mfumo wetu wa elimu unakidhi matarajio yake? Je, tunazalisha wasomi wenye moyo wa kujenga taifa au wasomi wenye ndoto za binafsi tu? Kama tunataka kumuenzi Mwalimu kweli, ni lazima tuutazame mfumo wetu wa elimu kwa jicho makini.

Elimu si tu kupata cheti. Elimu ni kujenga taifa. Elimu ni kuwa sehemu ya jamii na kushiriki kuibadilisha.

Katika falsafa ya Mwalimu Nyerere, tunapata mwanga wa safari yetu kama taifa, safari inayohitaji kila msomi kujitolea kwa manufaa ya jamii nzima.

Kazi Forums Ni chanzo chako bora cha makala na habari za kuaminika zilizochapishwa kwa weledi zaidi na uchunguzi wa kina.